Jumat, 02 Januari 2009

HOTUBA YA MHE. CAPT MST JAKA M MWAMBI BAOLZI WA TANZANIA NCHINI URUSI WAKATI WA SHEREHE YA MWAKA MPYA WA 2009 ILIYOFANYIKA UBALOZINI TAREHE 01/01/2009




Ndugu Wageni Waalikwa,

Mabibi na Mabwana.

Awali ya yote ninapenda tuungane kumshukuru Mwanyezi Mungu, Muumba wa vitu vyote vinavyoonekana na visivyoonekana, Mtoaji wa Mapaji na Rehema Ndogo Ndogo na Rehema Kubwa Kubwa, kwa Wema wake wa kutujailia pumzi ya kuishuhudia Siku hii kubwa ya kuzaliwa kwa Mwaka Mpya wa 2009. Tuendelee kuomba Baraka zake ili kama tulivyouanza, tuweze pia kuumaliza Mwaka huu tukiwa na afya njema, maisha marefu na mafanikio makubwa katika shughuli zetu za kila siku.

Leo ni siku kubwa kwetu sote. Ni siku ya kufanya tafakari binafsi. Kila mmoja bila shaka anatafakari yale yote aliyoyafanya katika mwaka uliopita na kujiwekea malengo ya mambo atakayotekeleza mwaka 2009. Bila ya kuwa na upeo wa kufikiri na kudurusu kwa kiwango fulani na kufanya tafakari ni sawa na kusema yaliyopita si ndwele, tugange yaliyopo na yajayo.

Kwa maisha ya binadamu hiyo ni kasoro. Ni lazima kutafakari yaliyopita, pengine kwa shukurani, tutazame hapa tulipo kwa kujiamini na kuweka mipango ya baadaye kwa matumaini.

Kamwe tusifanane na wale walevi waliokuwa wanabishana kuhusu jambo ambalo kila mmoja waokatika hali ya kawaida angekuwa na jibu. Hebu ngojeni nikusimulieni hadithi fupi ya walevi hao. Walevi wawili walipokuwa wanarudi kutoka kilabuni usiku, mmoja alimwambia mwenzake: “Leo jua linaonekana vizuri kweli kweli.”Mlevi wa pili alijibu, “Lile sio jua ni mwezi.” Basi waliendelea kubishana kuwa ni jua, ni mwezi, ni jua ni mwezi. Baadaye alitokea mlevi wa tatu. Wakamuuliza, “hebu tuambie lile ni jua au mwezi”, na kila mmoja alimwita mwenziwe kuwa ni mbishi sana. Yule mlevi wa tatu aliinua kichwa na kutazama juu kwa makini na kisha akasema, “Samahani mimi siishi katika eneo hili, kwa herini”.

Kwa hiyo, katika hali ya kawaida, na sisi hatuwezi kudiriki kusema hatuyajui mambo yanayotuhusu na kukwepa kuyafanyia tafakari yale yalitokea mwaka uliopita na kuweka malengo ya mwaka huu. Nafikiri ni jambo muhimu ambalo kila mmoja wetu ana wajibu ya kutathmini maisha yake yaliyopita, ya sasa, na ya baadaye.

Leo nina furaha zisizo kifani kwa sababu tofauti na tafrija zilizopita ambazo zilifanyika hapa Ubalozini, zilizokuwa zinahudhuriwa na watu mbalimbali, tafrija hii inahudhuriwa kwa sehemu kubwa na wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Urafiki cha Lumumba. Ninasema nina furaha kubwa kujumuika nanyi katika sherehe hii kwa sababu ni siku ya kufungua ukurasa mpya wa uhusiano na ushirikiano kati ya wanafunzi wa Chuo hicho na Ubalozi. Na tumefungue ukurasa mpya.

Nilianza kwa kuelezea umuhimu wa kufanya tafakari wa mambo tuliyoyafanya mwaka uliopita. Ni dhahiri kuwa nimeshika uongozi wa Ubalozi wetu na kurithi matatizo ya uhusiano hasi kati ya Ubalozi na wanafunzi wa chuo Kikuu cha Urafiki. Uchunguzi wa kina uliofanywa na Ubalozi imebainisha kuwa mbegu ya sumu hiyo mbaya ya uhusiano mbaya ilikuwa inapandikizwa na kuenezwa na wanafunzi wachache sana, ambao walitumia vibaya mwavuli wa uongozi wa TSU kuchochea migomo haramu, hata kwa wanafunzi wapya wanaoendele kuwasili na kujiunga na Chuo hicho.

Ndugu zangu, kila binadamu amekirimiwa na Mwenyezi Mungu karama ya utashi wa ufahamu wa mema na mabaya. Hivyo wote walioshiriki katika maandamano na migomo yote haramu walitenda makosa. Hukuna kisingizio chochote kwamba walifanya hivyo kwa kulazimishwa. Ninafahamu kuwa baadhi yenu hamkushiriki katika maandamano na migomo hiyo haramu. Hivyo hoja ya kulazimishwa kutenda kosa na kukubali kulitenda siyo hoja ya msingi.

Ni vizuri kila mmoja wenu aelewe kuwa ni wajibu wa Ubalozi wetu kushughulikia matatizo yenye maslahi kwa watanzania wote waishio katika nchi zote 12 za Uwakilishi. Wanafunzi ni sehemu ya jamii hiyo inayostahili kupata huduma zote muafaka kutoka Ubalozini. Lakini wakati huo huo ni vema pia kuelewa kuwa Ubalozi unafanya kazi zake kwa kuzingatia Makubaliano ya Kikonseli na Kidiplomasia ya Vienna ya Mwaka 1963, (the Vienna Convention on Consular and Diplomatic Relations). Kwa mujibu wa Makubaliano hayo, eneo la Ubalozi lina hadhi na heshima inayotambuliwa kimataifa. Balozi ana hadhi na heshima ya kumwakilisha Mheshimiwa Rais katika nchi zote hizo 12 za Uwakilishi. Hivyo, eneo la Ubalozi sio mahali pa kuchezewachezewa kama ambavyo baadhi yenu wamekuwa wakifanya. Ubalozini ni mahali pa kuheshimiwa. Na ni watanzania wenyewe wanaotakiwa kuuheshimu Ubalozi wao badala wa kuchafua hadhi yake.

Nimeeleza kuwa Ubalozi unafanya shughuli zake kwa mujibu wa Makubaliano ya Vienna na maelekezo mbalimbali kutoka kwa viongozi wa serikali yetu. Ubalozi haulazimiki kupokea maelekezo yo yote kutoka kwa Vyama vya Siasa. Sheria Na. 5 ya Vyama vya Siasa ya Mwaka 1992 inatoa fursa na uhuru kwa Mtanzania yeyote kujiunga na Chama chochote cha Siasa akipendacho. Lakini ninapenda kuonya kuwa kuutumia uhuru huo kwa kuutaka Ubalozi utimize majukumu yake kinyume na Makubaliano ya Vienna na kinyume cha maelekezo ya Serikali ni jambo lisilokubalika.

Ninapenda pia wanafunzi, hasa wa Chuo Kikuu cha Urafiki, waelewe kuwa dhana iliyojengeka miongoni mwenu kuwa hapa Ubalozi zipo fedha za wanafunzi na kuna mtu anayezishikilia badala ya kuwalipa ni dhana potofu. Ubalozi hauwezi kufanya kitendo cha ovyo kiasi hicho. Ni kutokana na dhana hiyo potofu wanafunzi wanapotaka kujua hatima ya malipo ya mikopo yao huja Ubalozini kwa makundi, jambo ambalo si lazima.

Ni vema nitumie fursa hii kukujulisheni kuwa nimetoa uamuzi wa kuruhusu kuingia ndani ya Uabalozi si zaidi ya wanafunzi wawili kwa wakati mmoja. Uamuzi huo unatokana na kitendo cha wanafunzi 35 waliogoma kutoka nje na kulala Ubalozini kwa siku nne tangu tarehe 5-8 Agosti 2008. Bila shaka sote tunaufahamu usemi kuwa “aliyeumwa na nyoka, ukiuona hata ujani ataukimbia.”

Kwa hiyo, kwa vile viongozi wenu TSU takriban wote wamerudishwa nyumbani, na kwa vile hata wangekuwapo tayari nilitoa agizo la kutowaruhusu kuingia ndani ya jingo la Ubalozi, hivyo ni vema mtumie haki yenu ya kikatiba kwa kuchagua viongozi wapya. Ninaelekeza kuwa viongozi watakaochaguliwa ni wale ambao watekeleza majukumu yao kwa mujibu wa Katiba yenu. Na iwapo Katiba yenu inatoa mwanya kwa viongozi kuchochea migomo, kujenga chuki na kutukana viongozi wa serikali na Ubalozi, au kuruhusu mawasiliano na Vyama vya Siasa, kama Katiba yenu ina kasoro hizo, ni vema kuifanyia marekebisho. Chagueni viongozi wenye staha, heshima, waadilifu na watakaowajibika kwa wanafunzi wote na sio kutumia madararaka yao ya uongozi vibaya kwa maslahi yao binafsi.

Ninarudia kueleza kuwa haipo haja ya wanafunzi kuja Ubalozini kwa makundi na kujazana nje ya Ubalozi. Utaratibu huo hauleti picha nzuri. Zaidi ya yote, mjue polisi sasa hawawaamini tena wanafunzi wa Chuo cha Urafuki ( Lumumba).Kila mnapokuja kwa makundi ndivyo na polisi nao huongeza idadi ya askari, hali ambayo haioneshi picha nzuri.

Kwa jumla, watumieni viongozi mtakaowachagua kuwasilisha Ubalozini matatizo yenu na kufuatilia matokeo yake. Sisemi kuwa mwanafunzi yeyote mwenye shida haruhusiwi kuja Ubalozini. La hasha! Ni ruhusa kufanya hivyo ili mradi tu uachwe mtindo wa kufika Ubalozini kimakundi. Hivyo, wanafunzi wa Mwaka wa Lugha ambao walichelewa kujaza fomu za mikopo au kwa sababu nyingine yo yote ile fedha zao za mikopo bado hazijaletwa, nao waelewe kuwa Ubalozi unafanya mawasilino na Bodi ya Mikopo ili kuhakikisha kuwa wanaharakisha kushughulikia mikopo ya wanafunzi hao. Fedha zao zikifika mara moja watajulishwa na kulipwa. Hivyo, haipo haja nao kuja kujazana nje ya Ubalozi kwa minajili au sababu hiyo hiyo.

Nimesema mengi, ingawa wanasiasa baada ya kusema maneno mengi ni kawaida yao kusema baada ya maneno hayo machache. Leo ni siku ya kufurahi. Tunafungua ukurasa mpya. Tupongezane kwa kujaliwa pumzi ya kuuona mwaka mpya.Tumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia pumzi hiyo.

Vimeandaliwa vinywaji na vyakula. Sipendi vyakula vipoe na vinyaji navyo vinadai kunywewa na hata mziki unadai kuchezwa! Basi tufurahi vizuri. Tusiwe kama jamaa mmoja aliyekunywa pombe kwenye tafrija kama hii hadi akaanguka na kuumia katika paja lake la uso. Jirani yake alimpa ushauri wa kukausha kdonda kwa kujimwagia whisky kidogo. Baada ya muda kidonda kiliendelea kutoka damu. Alipoulizwa kwa nini hakukikausha kwa kumwagia kidogo whisky kama alivyoshauriwa, alijibu kuwa, “kila nilipojaribu kuinua glasi mkono wangu, haukuweza kuinuka juu zaidi ya kuupita mdomo wangu!”

Baada ya kusema hayo machache, ninakutakieni heri na fanaka za Mwaka Mpya.

HAPPY NEW YEAR.

Mungu Ibariki Tanzania,

Mungu Ibariki Afrika,

Mungu Ubariki Ubalozi,

Mungu Ubariki Mwaka 2009.


CAPT MST JAKA M. MWAMBI

BAOLZI

MOSCOW-RUSSIA

Tidak ada komentar:

Posting Komentar