Jumat, 28 Agustus 2009

Michael Jackson 'aliuawa', afisa aeleza


Afisa mchunguzi wa vifo huko Los Angeles nchini Marekani ametangaza rasmi kuwa kifo cha Michael Jackson kilisababishwa na mtu mwingine, Jackson alifariki mwishoni mwa mwezi Juni.

Alieleza kuwa kifo chake kilisababishwa na kupewa dawa ya ganzi aina ya propofol, na nyingine ya kutuliza maumivu aina ya lorazepam.

Chembe chembe za dawa nyingine aina nne tofauti pia zilikutwa katika mwili wa mwanamuziki huyo.

Mwandishi wa BBC aliyeko Los Angeles anasema hitimisho hilo linaongeza uwezekano wa kufunguliwa mashtaka ya uhalifu dhidi ya madaktari waliokuwa wakimpatia Michael Jackson madawa hayo.

Kwa mujibu wa nyaraka zilizotolewa hivi karibuni na ofisa huyo mchunguzi wa vifo, daktari binafsi Conrad Murray, aliyekuwa akimtibu Bw Jackson, aliwaeleza polisi alimpatia mwanamuziki huyo dawa aina ya propofol kumsaidia apate usingizi. Dr Murray amekana madai ya uhalifu.

Mazishi ya mwanamuziki huyo yamepangwa kufanyika Septemba 3 katika eneo la Forest Lawn Memorial Park huko Glendale, kitongoji cha Los Angeles, katika shughuli itakayokuwa ya faragha.

Mazishi hayo awali yalipangwa kufanyika tarehe 29 Agosti - siku ambayo angekuwa hai angetimiza umri wa miaka 51.

Tidak ada komentar:

Posting Komentar