Minggu, 01 Februari 2009

Vikwazo dhidi ya Zimbabwe viondolewe


Rais Robert Mugabe wa Zimbabwe na Morgan Tsvangirai
Morgan Tsvangirai ataapishwa kama waziri mkuu chini ya serikali ya pamoja
Siku ya Jumamosi Afrika Kusini imetoa mwito kwa Marekani na mataifa ya Ulaya kuiondolea vikwazo vya kiuchumi Zimbabwe, wakati serikali ya rais Robert Mugabe inapojiandaa kugawanya madaraka na kiongozi wa upinzani.

Serikali ya Pretoria imesema inafaa mataifa ya magharibi kutoa nafasi hiyo ili kuiwezesha nchi hiyo jirani kuweza kukarabati mambo mengi yaliyokwenda mrama na kuifanya nchi hiyo maskini, yapata mwaka mmoja uliopita, kufuatia ubishi baada ya uchaguzi mkuu.

Miezi mingi ya mgogoro ilifikia kikomo Ijumaa iliyopita, wakati hatimaye kiongozi wa upinzani Morgan Tsvangirai alipokubali kuapishwa kama waziri mkuu, na vyama vyote kuanzisha mipango ya serikali ya pamoja.

"Kwa kuwas sasa (Morgan Tsvangirai) ameamua kuwa sehemu ya serikali hiyo ya pamoja...inawalazimu kusitisha vikwazo hivyo", alielezea Frank Chikane, mkurugenzi mkuu katika afisi ya rais wa Afrika Kusini.

Alielezea kupitia redio ya Afrika Kusini kwamba anatazamia mataifa ya Ulaya na Marekani, pamoja na nchi nyingine ambazo ziliiwekea vikwazo vya kiuchumi Zimbabwe, kuondoa vikwazo hiyo.

Mataifa ya Marekani na Uingereza yamekuwa yakiipinga vikali serikali ya Rais Robert Mugabe, na inaelekea mataifa hayo hayakutaka mara moja kuanza kushabikia mapatano hayo ya Ijumaa kwa haraka.

Tidak ada komentar:

Posting Komentar