Sabtu, 03 Oktober 2009

Wanachama wa CCM Arusha watimka kwenda TLP, CHADEMA

Wanachama wa CCM Arusha watimka kwenda TLP, CHADEMA
Hemed Kivuyo, Arusha

Hali `tete` imezidi kukikumba Chama Cha Mapinduzi (CCM) mkoani Arusha baada ya wanachama 100 wakiwamo baadhi ya viongozi wa mashina na matawi kukihama chama hicho kwasababu mbalimbali.

Hali hiyo imekuja siku chache baada ya mchakato wa kuwapata wagombea wa serikali za mitaa kumalizika na baadhi yao kudai hawakutendewa haki katika mchakato huo na hivyo kuhamia katika vyama vya upinzani.

Mmoja wa waasisi wa CCM Haruna Fundikira (90) alitangaza kukihama chama hicho na kujiunga na TLP akiwa na kundi la wanachama wenzake pamoja na mkewe kwa kile alichodai kuwepo kwa baadhi ya viongozi wasiokuwa na nia ya dhati ya kukiongoza chama hicho.

Hali hiyo imesababisha katibu mpya wa mkoa, Mary Chitanda na katibu wa wilaya Salimu Mpamba kuonekana kushindwa mapema jitihada zao za kutaka kukirejesha chama hicho katika kile walichodai kuwa ni ustawi na kuongeza idadi ya wanachama kisha kushinda chaguzi zijazo kwa kishindo.

Wakiongea kwa nyakati tofauti baadhi ya wanachama wa CCM mkoani hapa walisema, mpaka sasa hawajaona tofauti iliyoletwa na viongozi hao wapya zaidi ya kushuhudia wakiondokewa na wanachama na viongozi wao wa mitaa.

``Hatujaona mabadiliko yaliyodaiwa kuletwa na hawa viongozi wapya zaidi ni kuondoka kwa viongozi na wanachama na mpaka sasa hatujaona kitu kipya ``Alisema mmoja wa wanachama hao aliyezungumza na gazeti hili.

Katika kata ya sokoni inayoongozwa na diwani wa chama cha T.L.P zaidi ya wanachama 30 wa CCM walihamia katika vyama vya Chadema na T.L.P kwa madai ya kutotendewa haki katika kura za maoni.

Akizungumza na Mwananchi Jumapili Katibu wa Wilaya wa CCM, Salim Mpamba alisema kuwa anachofahamu ni kuhama kwa mmoja wa wenyeviti wa chama hicho pamoja na muasisi wa chama hicho kata ya Levolosi na kwamba jambo hilo halimtishi.

Katibu huyo wa Wilaya aliongeza kuwa kuhama kwa watu hao siyo mwisho wa chama hicho na kwamba, wataendelea kukusanya wanachama wapya na hatimaye kuibuka na ushindi wa kishindo.

Tidak ada komentar:

Posting Komentar