Sabtu, 25 April 2009

Shirika la Fedha la Dunina kuipa Tanzania Sh340 bilioni

SHIRIKA la Fedha la Duninai (IMF), linatarajia kuipa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania dola za Marekani 340 milioni (zaidi ya shilingi 340 bilioni), kwa ajili ya kukuza urari wa biashara (Balance of Payment).

Fedha hizo ambazo zitatumiwa na Benki Kuu ya Tanzania (BoT), kukuza urari huo zinatarajiwa kutolewa na IMF mwanzoni mwa mwezi wa Mei, mwaka huu zinalenga kukabiliana na makali ya mtikisiko wa kiuchumi.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana kwa vyombo vya habari na Waziri wa Fedha na Uchumi, Mustafa Mkulo aliyeko Washington DC, Marekani jana, fedha hizo zitatumiwa na BoT, kuziba pengo ambalo litatokea katika akiba ya fedha ya taifa(Government Reserve).

“Fedha hizi zitasaidia Tanzania hasa katika kipindi hiki kigumu cha mtikisiko wa uchumi, kwani ilikadiriwa kuwa hadi kufikia Juni mwaka huu, Tanzania isingekuwa na uwezo wa kuagiza bidhaa kutoka nje ya nchi, kama vile madawa na chakula kutokana na kukosa fedha za kigeni,” alisema Waziri Mkulo.

Wakati huo huo, Mkulo alisema kuwa Benki ya Dunia (WB) imekubali kuipatia Tanzania dola za Marekani 970 milioni, kwa ajili ya kusaidia Bajeti ya Serikali kwenye maeneo ya kilimo, umwagiliaji na mradi wa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF).

“Kati ya fedha hizo dola 750 milioni zitatolewa katika kipindi cha fedha cha mwaka wa fedha 2009/2010,” alisema Mkulo.

Alisema mgawanyo wa fedha hizo utakuwa ni dola milioni 200 ni kwa ajili ya Bajeti ya Serikali, dola milioni 160 kilimo, ununuzi wa mbolea, mbegu bora na umwagiliaji. Dola milioni 30 zitakwenda kusaidia mradi wa TASAF.

Mkulo alisema athari za mtikisiko huo zinatarajiwa kuchukua kati ya mwaka mmoja na nusu hadi miwili.

“Katika kujinasua na msukosuko huo Tanzania imekubaliwa na Benki ya Dunia(WB) kukopa katika vyanzo vya kibiashara kama vile Benki ya Kimataifa ya Ujenzi na Maendeleo (International Bank for Reconstruction and Development-IBRD), alisema Mkulo.

Tidak ada komentar:

Posting Komentar