Minggu, 01 Maret 2009

Israel yapaswa kuheshimu makubaliano yaliyotangulia

Israel yapaswa kuheshimu makubaliano yaliyotangulia

Mkuu wa sera za nje wa Umoja wa Ulaya Javier Solana amesema serikali yo yote ile itakayoundwa nchini Israel,inapaswa kuendelea kuheshimu makubaliano yaliyopatikana wakati wa serikali zilizotangulia.

Solana,anatazamia kuwa serikali itakayoundwa Israel na Benjamin Netanyahu wa chama cha Likud cha mrengo wa kulia,ataendelea na mchakato wa amani kupata suluhisho la mataifa mawili katika Mashariki ya Kati.

Baada ya kukutana na Rais wa Wapalestina Mahmoud Abbas mjini Ramallah kwenye Ukingo wa Magharibi,Javier Solana alisema,ni matumaini yake kuwa serikali ijayo nchini Israel itaheshimu makubaliano yaliyopatikana pamoja na Wapalestina na itasitisha harakati za ujenzi wa makaazi ya walowezi wa Kiyahudi katika Ukingo wa Magharibi.

Solana ametembelea Israel na maeneo ya Wapalestina kujitayarisha kwa mkutano wa wafadhili utakaoanza siku ya Jumatatu nchini Misri katika juhudi ya kusaidia ujenzi upya kwenye Ukanda wa Gaza.Msaada huo wa fedha hautotolewa kwa Hamas kundi linalodhibiti Ukanda wa Gaza,bali utapitia Utawala wa Wapalestina na utagawanywa kwa kushirikiana na mashirika ya kimataifa.

Tidak ada komentar:

Posting Komentar